Mkuu wa Mkoa wa Lindi Mhe. Zainab Telack, ametangaza kuanza kwa kambi maalumu ya Upasuaji wa Mabusha itakayofanyika kuanzia tarehe 9 hadi 25 Februari, 2026 katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Lindi – Sokoine. Akizungumza na waandishi wa habari leo Februari 6, 2026, ofisini kwake, Mhe. Telack amesema kambi hiyo inalenga kuwahudumia wananchi wanaosumbuliwa na matatizo ya mabusha, ambapo jumla ya wananchi 500 wanatarajiwa kunufaika na huduma hiyo bila malipo. Mhe. Telack amebainisha kuwa Kambi hii ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuboresha huduma za afya na kudhibiti Magonjwa Yasiyopewa Kipaumbele ikiwemo na Mabusha. Aidha, ameeleza kuwa gharama zote za uchunguzi, upasuaji pamoja na chakula kwa wagonjwa watakaolazwa zitagharimiwa kikamilifu na Serikali. Aidha, Mhe.Telack amewahimiza wananchi wa Mkoa wa Lindi kujitokeza kwa wingi na kuwahamasishana kufika hospitalini kwa ajili ya kupata huduma na kuongeza kuwa kambi hiyo itahusisha madaktari bingwa kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa kushirikiana na wataalamu wa afya wa Mkoa wa Lindi, hatua itakayohakikisha huduma bora na salama kwa wagonjwa wote. Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Dkt. Kheri Kagya, ametoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi katika Kambi hiyo ili kupata huduma stshiki na kuongeza kuwa Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Lindi Sokoine imejipanga kikamilifu kuhakikisha wananchi wanapatiwa huduma ya upasuaji bila gharama yoyote.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Lindi
Sanduku la Posta: P.o Box 1054 Lindi
Simu: 023-220-2098
Rununu:
Barua pepe: ras.lindi@tamisemi.go.tz
Hati miliki ©2017 Lindi . Haki zote zimehifadhiwa.